MAKAMU wa Rais, Dk Mohammed Gharib Bilal
MAKAMU wa Rais, Dk Mohammed Gharib Bilal amevionya vyama vya siasa nchini na kuwataka viongozi wake kuacha kuwapandikiza wananchi mbegu za chuki na uhasama kwa uroho wa madaraka.
Alisema hayo wakati akifungua Kongamano la Miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar mjini hapa, ambalo lililenga zaidi kuzungumza mwelekeo wa uchumi na ustawi wa jamii.
Alisema vipo vyama vya siasa, visivyokuwa na ushawishi Zanzibar, vimekuwa vikiendesha siasa za chuki, zenye mwelekeo wa kuwagawa Watanzania, ambao kwa zaidi ya miaka 50 sasa wanaishi ndani ya Muungano huo kwa ushirikiano mkubwa.
“Dhambi ya utengano ni kubwa na watakaoathirika ni wananchi wetu, ambao wananufaika sana na faida za Muungano kijamii na kiuchumi,” alisema.
Alielezea kusikitishwa na tabia ya baadhi ya wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kususia vikao bungeni mjini Dodoma huku baadhi yao wakitoa kauli za chuki zenye mwelekeo wa kukebehi viongozi wakuu wa nchi, ikiwemo Waasisi wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na Abeid Amaan Karume.
Alisema kauli hizo, hazikubaliki na si za kiungwana kwa wananchi wa Tanzania, ambao kwa muda mrefu wanaishi katika mazingira ya amani na utulivu mkubwa.
“Nimesikitishwa sana na tabia ya hawa waliotoka nje ya kikao cha Bunge Maalumu la Katiba huku wakitoa kauli za matusi zenye kuwakebehi viongozi wakuu wa nchi,” alisema Bilal.
Alisema Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, umepata baraka ya wananchi, ambao walihojiwa na kupatikana ridhaa yao.
Post a Comment