Imeandikwa na Regina Kumba
WAKALA wa Barabara Tanzania (Tanroads) imesema kufikia mwaka 2018 mamlaka hiyo itakuwa imekamilisha utengenezaji wa barabara katika kiwango cha lami kuunganisha nchi nzima.
Mpango huo ulielezwa jana na Mhandisi Mipango wa Mkoa wa Dar es Salaam, John Ngowi jijini Dar es Salaam wakati wakizungumzia mafanikio, changamoto na mikakati ya Tanroads.
“Mpango uliopo kwa serikali na Tanroads ni kuunganisha barabara kuu na nchi nzima kwa kiwango cha lami kufikia mwaka 2018 itakuwa imekamilika,” alisema Ngowi.
Akizungumzia barabara zinazoharibika mara tu baada ya ujenzi au kabla hata ujenzi haujakamilika, alisema tatizo hilo linapojitokeza kama ilivyo katika barabara ya Kilwa jijini Dar es Salaam, mkandarasi anatakiwa kurudia barabara hiyo mara moja kwa gharama zake na sio gharama za Serikali.
Alisema kutokana na mapungufu hayo ambayo hujitokeza, muda wa maangalizi umeongezwa hadi miaka mitatu ili kuendelea kutazama ubora wa barabara ikiendelea kukaguliwa na Tanroads mpaka itakapojiridhisha.

Post a Comment