Home » » CUF KUTOWEKA MGOMBEA UCHAGUZI MDOGO JIMBO LA KALENGA

CUF KUTOWEKA MGOMBEA UCHAGUZI MDOGO JIMBO LA KALENGA

Written By JAK on Tuesday, February 11, 2014 | 8:22 PM


Mbio za kuwania ubunge katika Jimbo la Kalenga unabaki kwa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na Chama Cha Mapinduzi (CCM), baada ya Chama cha Wananchi (CUF) kuthibitisha kutosimamisha mgombea.
Naibu Mkurugenzi wa Habari na Uhusiano wa Umma wa CUF, Abdul Kambaya, amesema chama chake hakina mpango wa kusimamisha mgombea katika jimbo hilo na kwamba hivi sasa wanaandaa mikutano ya kuimarisha chama chao.
“Mpaka sasa CUF haina mpango wa kusimamisha mgombea ubunge Kalenga… kwa sasa tunaandaa kikao cha Kamati Tendaji kitakachokaa kati ya Februari 15 na 16 mwaka huu ili kujadili masuala mbalimbali,” alisema Kambaya.
CHADEMA imepanga kumtangaza mgombea wa kiti hicho wakati wowote baada ya Kamati Kuu ya chama hicho kuketi mwishoni mwa wiki hii kwa ajili ya kuteua jina la mgombea.
“Kwa sasa chama kinakusanya fomu za waliojitokeza kugombea jimbo hilo… hadi sasa tunaendelea na zoezi hilo, mwamuzi wa mwisho ni kamati kuu itakayoketi mwisho wa mwezi huu kwa ajili ya uteuzi wa jina hilo,” alisema Ofisa Habari wa Chama hicho, Tumaini Makene.
Juzi CCM ilimtangaza Godfrey Mgimwa, mtoto wa aliyekuwa mbunge wa Kalenga na Waziri wa Fedha na Uchumi, marehemu  William Mgimwa, kugombea katika uchaguzi mdogo, ambao kampeni zake zitaanza rasmi Februari 19, mwaka huu.
Mgimwa alichaguliwa kwa kura 348 za maoni za wajumbe 708 kati ya wajumbe halali 816 wa CCM katika mkutano mkuu wa jimbo hilo, na aliibuka kidedea kati ya wagombea tisa waliokuwa wakiwania nafasi hiyo.
Share this article :

Post a Comment

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. New EAC Blog - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger