Home » » DAWA ZA KULEVYA ZACHAFUA MAHAKIMU,MAJAJI

DAWA ZA KULEVYA ZACHAFUA MAHAKIMU,MAJAJI

Written By JAK on Wednesday, November 6, 2013 | 11:34 AM

http://in2eastafrica.net/wp-content/uploads/2013/08/Esther-Bulaya.jpg
MBUNGE wa Viti Maalumu, Esther Bulaya (CCM) amesema juhudi za Serikali kupambana na dawa za kulevya, zinazimwa na baadhi ya watendaji wasio waaminifu katika Ofisi ya Mwendesha Mashitaka (DPP), mahakimu na majaji.

Amesema watendaji hao wasio na uzalendo, wanashirikiana na watuhumiwa wa dawa za kulevya wenye kesi, kupanga jinsi ya kushinda kesi kwa kuwapa taarifa za siri zinazohusu ushahidi na jinsi ya kuuharibu.

Bulaya akitoa maelezo binafsi bungeni juzi, alisema mtandao uliopo katika Ofisi ya DPP umekuwa ukituhumiwa kufanya njama za kushirikiana na baadhi ya watumishi wa Mahakama, hasa majaji, kuhamisha kesi na kupeleka kwa majaji wanaodaiwa kuhusika na mtandao huo.

“Sina haja kutaja majina ya majaji hapa, baadhi yao wanafahamika na wengine wametajwa mara kadhaa na vyombo vya habari, lakini kwa kutumia mtandao huo, baadhi yao wamekuwa wanatafsiri sheria jinsi wanavyotaka na kuwapa dhamana watuhumiwa wa kesi za dawa za kulevya ambazo hazina dhamana,” alieleza Bulaya.

Akitoa mfano wa kesi hizo, Bulaya alitaja kesi namba 6/2011 ya Jamhuri dhidi ya Fred William Chonde na wenzake, ambao walikutwa na kilo 179 za dawa za kulevya aina ya heroine yenye thamani ya Sh bilioni 6.5
Alisema washitakiwa hao, walifikishwa mahakamani kwa tuhuma za kusafirisha dawa za kulevya ambapo kwa mujibu wa sheria, hazina dhamana. Alitaja sheria zinazozuia dhamana katika makosa hayo kuwa ni Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai, kifungu cha 148 (5), (a) (iii) na Sheria ya Kuzuia Usafirishaji wa Dawa za Kulevya kifungu cha 27(1) (b).

Bulaya alisema kwa tafsiri yoyote, Jaji hakupaswa kutoa dhamana kwa kuwa kosa la kusafirisha dawa za kulevya zenye thamani inayozidi Sh milioni 10, halina dhamana.

Pamoja na sheria hizo kutomwachia Jaji uhuru wa kutoa dhamana au la, Bulaya alisema Mahakama ilitoa dhamana na washitakiwa hao raia wa Pakistani, kwa sasa hawapo tena nchini, wametoroka. Kesi nyingine aliyoitaja ni ya R.V. Mwinyi Rashid Ismail na Mkoko namba KLR/IR4143/2011, ambapo mshitakiwa aliomba dhamana Mahakama Kuu, wakati kesi ilikuwa bado Mahakama ya Kisutu.

Katika kesi hiyo kwa mujibu wa Bulaya, jalada la kesi hiyo lilipofikishwa Mahakama Kuu kwa ajili ya dhamana, wakati kesi ya msingi iko Kisutu, Wakili wa Serikali alimwambia Jaji kuwa anataka kuifuta.

Waadhibiwe Kutokana na udhaifu huo, Bulaya aliitaka Serikali kufanya mabadiliko ya Sheria ya Dawa za Kulevya na kuanzisha Mahakama Maalumu ya kushughulikia wahalifu wa dawa hizo.

Aliwasilisha maelezo hayo chini ya kanuni ya 28 (8) ya Bunge toleo la mwaka 2013, kuhusu tatizo sugu la uagizaji, uuzaji na usafirishaji wa dawa hizo linaloongezeka kwa kasi kubwa nchini kwa lengo la kuitaka Serikali ichukue hatua hizo.

Bulaya alisema ni wakati mwafaka kutoa maelezo hayo, ili Bunge na Serikali wapate fursa ya kuona uzito wa tatizo la dawa za kulevya, kutokana na ukweli, kwamba katika miaka ya karibuni tatizo hilo limeongezeka kwa kasi ya ajabu hali inayosababisha athari kubwa za kiuchumi, kijamii na kiafya nchini, huku kundi kubwa linaloathirika likiwa la vijana.

Utafiti Bulaya alisema utafiti wa hivi karibuni wa Umoja wa Mataifa (UN) unaonesha kuwapo ongezeko kubwa na la kutisha, la matumizi ya dawa hizo aina ya heroin kwa njia ya kujidunga katika Kenya, Libya, Mauritius, Shelisheli na Tanzania.

Akinukuu ripoti mpya ya hivi karibuni ya ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kupambana na Mihadarati na Uhalifu (UNODC), alisema imetamka bayana, kwamba Tanzania ina hali tete katika Afrika Mashariki na mkoa wa Tanga umo hatarini zaidi.

Wabunge waja juu Jana Mbunge wa Simanjiro, Christopher ole Sendeka (CCM) aliomba Mwongozo wa Spika kuhusu maelezo binafsi ya Bulaya, juu ya utendaji duni wa baadhi ya Mahakama na vyombo vingine vya ulinzi na usalama.

Alitaka Serikali itoe jibu kuhusu hukumu za washitakiwa wa kesi za dawa za kulevya na mustakabali wa Watanzania kwa usumbufu wanaopata kimataifa hivi sasa.

Akijibu hoja hiyo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Bunge, William Lukuvi, alisema tayari Serikali inafanyia kazi suala hilo.

“Serikali inajiandaa kutoa kauli yake bungeni kabla ya Bunge kwisha kupitia Waziri wa Katiba na Sheria kuhusu ufafanuzi wa namna inavyojipanga kutekeleza hili, yaliyozungumzwa na Bulaya ndiyo tunayafanyia kazi sasa, pia kuunda chombo kipya.Hata sisi tumejipanga na pia tutafafanua hoja ya Bulaya,” alisisitiza Lukuvi.

Pamoja na ufafanuzi huo, Mbunge wa Mwibara, Kangi Lugola (CCM), aliomba Mwongozo akihoji kwa nini Bunge lisitenge muda kujadili suala muhimu kama hilo la dawa za kulevya kwa kutumia mamlaka ya kikanuni ya Spika.

Alisema Bunge limekuwa likipoteza muda na kufanya mambo yasiyo muhimu ikiwemo kuruhusu hata watu wasiohusika wala kuruhusiwa kuingia ndani ya Bunge kama wachezaji wa mpira na wanafunzi waliofaulu vizuri, hivyo likubali masuala kama hayo ya dawa za kulevya yajadiliwe.

Hata hivyo, Naibu Spika Job Ndugai alimweleza Lugola kuwa, kanuni inaeleza wazi, kuwa ni kwa idhini ya Spika ndipo maelezo binafsi yanaweza kujadiliwa, na akafafanua kuwa Spika juzi aliona jambo hilo lisijadiliwe na huo ndio uamuzi wa mwisho.

Share this article :

Post a Comment

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. New EAC Blog - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger