Na Daniel Mjema,Mwananchi
Kwa ufupi
Mume wa mwanamke huyo, Jerome Mushi anasema watekaji hao
walikuwa na bastola, pingu na redio ya upepo na wamechukua Dola 11,000.
Moshi. Polisi imemtia mbaroni mtuhumiwa muhimu katika tukio
la mwanamke mmoja mjini Moshi aliyetekwa nyara na watu wasiojulikana na kwenda
kutelekezwa jijini Dar es Salaam.
Mwanamke huyo alichukuliwa na watu waliojitambulisha kuwa ni
askari wa upelelezi kutoka Dar es Salaam na kwamba, walikuwa wametumwa
kumkamata kwa tuhuma za kuuza dawa za kulevya.
Kamanda wa Polisi Mkoa Kilimanjaro, Robert Boaz alisema
mtuhumiwa huyo muhimu (jina tunalo) alikamatwa Dar es Salaam na kusafirishwa
hadi Moshi mwishoni mwa wiki iliyopita. Tukio hilo lilitokea Oktoba 13 mwaka
huu eneo la Soweto NHC, watu hao walimchukua mwanamke huyo, Asha Amini hadi Dar
es Salaam na kumpora Dola 11,000 za Marekani.
Boaz alisema aliyetoa taarifa hizo polisi, ni Jerome Mushi
na alijitambulisha kuwa ni mume wa mwanamke huyo.
“Aliporudi nyumbani (Mushi) hakumkuta mkewe akaambiwa
amekamatwa na polisi na amepelekwa Kituo Kikuu akaamua kwenda hadi kituoni
wakamwambia hakuna tukio kama hilo,” alisema Boaz.
Kamanda Boaz alisema jalada la uchunguzi lilifunguliwa na
siku hiyo hiyo watu walioondoka na mwanamke huyo, walimpigia simu mumewe
wakitaka walipwe Sh2 milioni.
Hata hivyo, Boaz alisema watu hao walimwachia huru mwanamke
huyo eneo la Bunju Dar es Salaam bila kumdhuru na kumpa Sh50,000 za nauli ya
kumfikisha katikati ya jiji.
Kwa upande wake, Jerome Mushi alisema waliomchukua mkewe
walikuwa na bastola moja, pingu mbili na redio moja ya upepo na walichukua dola
11,000 za Marekani.
Post a Comment