Home » » SUMAYE AMWUNGA MKONO KIKWETE

SUMAYE AMWUNGA MKONO KIKWETE

Written By JAK on Wednesday, November 6, 2013 | 11:56 AM



http://www.wavuti.com/uploads/3/0/7/6/3076464/964096818.JPG
              
ALIYEKUWA Waziri Mkuu, Frederick Sumaye, amesema wanachama wa CCM na wananchi wamepata matumaini mapya, kwa kauli ya Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete, ya kutaka watoa rushwa ndani ya chama hicho washughulikiwe.

Akizungumza jana na waandishi wa habari Dar es Salaam, Sumaye alisema kauli ya Rais Kikwete dhidi ya rushwa ndani ya CCM haitapotea hewani; bali itatekelezwa na italeta mabadiliko makubwa katika vita dhidi ya rushwa nchini na ndani ya chama hicho ambako alidai rushwa ni tatizo sugu.

“Mwenyekiti wangu nakupongeza sana sana kwa kukemea rushwa na ninakuunga mkono katika vita hii na ninaamini unajua kuwa mimi ni askari wako mmojawapo wa mstari wa mbele kupambana na tatizo hilo,” alisema Sumaye.

Sumaye alisema kwa vile Mwenyekiti amekabidhi jukumu la utekelezaji kwa Makamu wake wa Bara, Phillip Mangula, ambaye anajulikana kwa ujemedari imara katika vita dhidi ya rushwa, ni imani ya wanachama kwamba hatalionea haya suala hilo.

“Tunaamini kuwa Mangula hutaangalia sura ya mhusika wakati wa kuchukua hatua, maana ni kweli usiofichika wengi wa watoa rushwa ni watu wazito kwa kila namna,” alisema na kuongeza kuwa Sekretarieti na Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, wanapaswa kumpa Mangula ushirikiano usioyumba wakati wa kutatua tatizo hilo la rushwa ndani ya CCM.

Kwingine Lakini licha ya pongezi hizo kwa Rais Kikwete, Sumaye pia alihadharisha kuwa rushwa haiko ndani ya CCM peke yake, bali iko katika vyama vingine vya siasa, katika taasisi zinazojitegemea, serikalini na maeneo mengine mengi nchini.

“Kama Mwenyekiti alivyomwagiza Makamu wake kushughulikia rushwa CCM, namwomba Mwenyekiti asikomee hapo, bali aendelee kushughulikia rushwa katika Serikali na vyombo vyote vilivyoko chini ya Serikali,” alisema Sumaye.

Aliongeza kuwa katika vita ya rushwa, nchi itashinda iwapo askari wote watashikamana na kuunganisha nguvu pamoja.

“Ni vita kali, kubwa na ya hatari, lakini tukiwa pamoja tutashinda kwa uhakika. Alipoulizwa maoni yake kuwa iwapo watoa rushwa hao wakiteuliwa kupeperusha bendera ya chama chake katika uchaguzi matokeo yake yatakuwaje? Sumaye alisema iwapo chama kitapitisha majina ya watoa rushwa kwa kufumbia macho suala hilo, ni wazi kitaanguka.

“Siamini kama watapitisha watoa rushwa wanaonunua watu wengine, CCM itaepuka hilo, ila wakifumbia macho wajue tutaanguka katika uchaguzi kwani wananchi wamechoshwa na kelele za rushwa,” alisisitiza Sumaye.

Alisema anaamini watoa rushwa hawatapitishwa, kwani kati ya viongozi wa juu wa CCM, hakuna anayetaka chama kianguke katika uchaguzi mkuu ujao.

Alitishia kuwa iwapo watoa rushwa watapitishwa, hatathubutu kukaa nao, maana ni waovu ambao wananunua watu wapate madaraka. Sumaye alisema wana CCM wote wanapaswa kusema rushwa ni adui wa haki, kwani unapompa mtu rushwa ujue kuna anayedhulumika na kuumia na hiyo rushwa iliyotolewa.

Alisema rushwa inahamisha uhalali kwa anayestahili na kupewa asiyestahili na katika mchakato huo, mtoa rushwa anatenda dhambi ya kudhulumu haki kwa anayestahili.

"Unapofanya ufisadi kwa mradi wa Serikali, unaumiza Taifa katika siku zijazo kwa kuruhusu kiharusi cha uchumi na huduma kwa jamii," alisema Sumaye ambaye pia jana alitumia mkutano wake kuelezea mchezo mchafu unaofanywa na wanasiasa wenzake katika kuchafuana katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu 2015.

Jumuiya Akizungumzia suala la Tanzania kutengwa katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Sumaye alisema itakuwa ni makosa makubwa iwapo Tanzania itaamua kujiondoa. Alisema Jumuiya ya sasa wakati inaundwa, ilishirikisha wananchi katika hatua zote kabla ya viongozi wakuu wa nchi tatu kusaini makubaliano.

Alikumbusha, kuwa duniani kote nchi zinafirikia kuungana, ili kujiongeza nguvu, hivyo suala la Tanzania kuondoka kwenye Jumuiya hiyo yeye halishabikii hata kidogo. Alihoji wanaoangalia uwezekano wa kuunda ushirikiano na Jamhuri ya Kidemokrsia ya Congo (DRC), wajiulize kuwa nchi hiyo tangu ipate uhuru ni lini imekuwa na amani.

“Hivi sisi ndio mwarobaini wa kutuliza vurugu za DRC, nani kasema hawa majirani zetu si muhimu kwa sasa?” Alihoji Sumaye. Alisema kama suala ni ardhi, si dhambi kwa Wakenya kuimiliki, wakati ameshuhudia Kilosa kuna maeneo makubwa na wamemilikishwa Wachina.

“Kwa nini ni haramu kwa Wakenya? Nenda Arusha, ardhi yote imechukuliwa na wageni, na si kwa sababu ya EAC, iweje leo tuogope?” Waziri Mkuu huyo mstaafu, alisema huu si muda wa kuangalia nyuma, bali kusonga mbele kwa kuimarisha uchumi ikiwa ni pamoja na kuboresha bandari na reli.

Alisema bahati mbaya bandari hazifanyi kazi kwa ufanisi mkubwa, lakini kama Serikali itajipanga kuboresha bandari za Tanga, Mtwara na Dar es Salaam, uchumi wa nchi utaimarika zaidi. Alisema nchi ambazo hazina bahari, ndizo zitakazoifanya Tanzania isonge mbele kiuchumi kwa kutumia bandari zake kupitisha mizigo yao.

Alisema hoja hiyo inayoibuliwa sasa, inamuuma sana kwani walihangaika kuanzisha Jumuiya hiyo kwa kushirikisha wananchi na akahoji; “Iweje leo tuivunje miaka michache tu baada ya kuundwa? “Samahani kwa hili sikubaliani na msimamo wa kujiondoa, eti sisi ndio tutatoa talaka, nchi zote hizi ziko sawa hakuna wa kutalikiwa wala wa kutoa talaka,” alisema.

Hivi karibuni Wabunge waliitaka Serikali ijiondoe EAC kwa maelezo kuwa inatengwa na viongozi wa nchi za Kenya, Rwanda na Uganda.

Hata hivyo, Waziri Sitta alisema wakati ukifika, watatoa tamko na Tanzania ndio nchi kubwa hivyo kama ni talaka ndiyo itakayotoa kwa nchi hizo akipinga kauli ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe ambaye alitaka Tanzania ipewe talaka. Pia kumekuwa na taarifa kuwa Tanzania inaangalia uwezekano wa kuunda Jumuiya nyingine na nchi za DRC na Burundi.

Share this article :

Post a Comment

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. New EAC Blog - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger